Waandishi wa Habari Zanzibar Watakiwa Kuandika Habari za Takwimu Zinazoleta Suluhu kwa Jamii

Na Maryam Nassor

WAANDISHI wa habari nchini wametakiwa kuzingatia matumizi ya takwimu katika uandishi wao ili kuzalisha habari zenye ushahidi, zinazoibua changamoto na kupendekeza suluhu zenye manufaa kwa jamii.

Wito huo ,umetolewa na Afisa Habari na Mawasiliano wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ), Khairat Ali, wakati wa kufunga mafunzo ya siku mbili yaliyowakutanisha waandishi wa habari 20 kutoka  vyombo mbali mbali vya habari kisiwani Unguja.

Khairat amesema ,mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo waandishi wa habari katika kuandika habari zinazozingatia takwimu, haki za wanawake katika uongozi, haki za kidemokrasia na uandishi wa habari za tija zinazochangia maendeleo ya jamii.

"Tumewafundisha masuala ya takwimu kwa sababu tunataka kuona jitihada zetu katika kushughulikia masuala ya wanawake na uongozi zimefikia wapi, zimeleta mafanikio kwa kiwango gani, na jamii imezipokea kwa namna gani," amesema Khairat.

Kwa upande wake, mkufunzi wa mafunzo hayo, Dk. Imane Duwe, amesema mafunzo hayo  yalijikita katika uandishi wa habari unaotoa suluhu (Solutions Journalism) pamoja na uandishi unaotumia takwimu kuonyesha picha halisi ya changamoto na mafanikio yaliyopo katika jamii.

Amesema, waandishi wa habari wanapaswa kutumia takwimu kama nyenzo ya kuongeza uwajibikaji na kuangazia viongozi na watu wanaotoa huduma muhimu kwa jamii, hususan wanawake waliopo katika ngazi za chini za uongozi ambao mara nyingi hawapati kutambulika licha ya mchango wao mkubwa.

Aidha, amewasisitiza washiriki kuhakikisha makala watakazoandika zinaunganisha takwimu sahihi na mapendekezo ya suluhu ili kusaidia jamii na watunga sera kufanya maamuzi yenye tija.

Naye mjumbe wa TAMWA ZNZ, Bi. Shifaa Said, amewataka waandishi wa habari kuendelea kuzingatia maadili ya taaluma na sheria za nchi wanapotekeleza majukumu yao ili kulinda taaluma yao na kuepuka migogoro ya kisheria.

Amesema  kuwa,  ni muhimu vyombo vya habari kuwaibua wanawake waliopo katika nafasi mbalimbali za uongozi wa ngazi za jamii ambao kazi zao hazijulikani kwa wananchi, licha ya mchango wao mkubwa katika maendeleo.

Kwa upande wao, washiriki wa mafunzo hayo, Hadija Juma na Zurima Ramadhan, wameishukuru TAMWA ZNZ kwa kuwawezesha kushiriki mafunzo hayo, wakisema yamewaongezea ujuzi wa kuandika habari zinazotumia takwimu na kutoa suluhu kwa changamoto zinazoikabili jamii.

Mafunzo hayo ya siku mbili , yameandaliwa na TAMWA ZNZ  kwa  waandishi wa habari 30, ambapo 20 walitoka Unguja na 10 kutoka Pemba. Yalilenga kuimarisha uwezo wa waandishi katika uandishi wa habari za tija, matumizi ya takwimu na mbinu za uandishi unaotoa suluhu kwa maendeleo ya jamii.




 

No comments

Powered by Blogger.