MIMBA ZA UTOTONI ZINAENDELEA KUWANYIMA WASICHANA NDOTO ZAO.
Ukosefu wa elimu ya Afya ya uzazi inachangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa mimba za utotoni hasa maeneo ya vijijini.
Na Maryam Nassor
Kila mwaka, wasichana milioni 21 wenye umri wa kati ya
miaka 15 hadi 19 wanapata ujauzito katika nchi zinazoendelea
Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Afya Duniani (
WHO) ya mwaka 2020 inaonesha asilimia kubwa , ya matukio hayo hutokea katika nchi za Afrika, Kusini
mwa Jangwa la Sahara ambako viwango vya
uzazi kwa wasichana na wanawake vinazidi
kuwa juu.
Kwa hapa Tanzania, takwimu zinaonesha kuwa tatizo la mimba za utotoni
bado linaendelea kuwa changamoto kubwa, inayowakabili wasichana wengi nchini.
Kwa mujibu wa ripoti ya Utafiti wa Afya na Viashiria vya Malaria Tanzania
(TDHS-MIS) ya mwaka 2015/2016,.
Takribani asilimia 27 ya
wasichana wenye umri wa miaka 15 hadi 19 tayari walikuwa wameanza kuzaa au
walishawahi kupata ujauzito, hali inayochangia kuongezeka kwa idadi ya
wanafunzi wanaoacha shule na kukosa fursa za kutimiza ndoto zao za maisha.
Kwa mujibu wa UN Women ,katika ripoti yake ya
mwaka 2025 kuhusu haki za wasichana balehe duniani, mimba za utotoni
zinaendelea kuwa moja ya vikwazo vikubwa kwa maendeleo ya mtoto wa kike, kwani
huwanyima wasichana haki ya elimu, afya bora na ushiriki duni katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.,
Shirika hilo, linaeleza kuwa
wasichana wanaopata ujauzito katika umri mdogo wako katika hatari kubwa ya
umaskini, ukatili wa kijinsia pamoja na kupata changamoto za afya ya uzazi.
Kwa hapa Zanzibar , Katika baadhi ya maeneo ya
vijijini, wasichana wengi wamejikuta wakiacha masomo kutokana na ujauzito wa
mapema, huku wengine wakikumbana na changamoto za kiafya, kisaikolojia na hata
kutengwa na jamii.
Akizungumza na mwandishi wa Makala hii , msichana mdogo Amina (si jina lake halisi), mwenye umri wa miaka 16 kutoka kijiji cha Matemwe wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja , anasema maisha yake yalibadilika ghafla baada ya kupata ujauzito akiwa mwanafunzi wa kidato cha pili mwaka 2024.
“Nilikuwa nina ndoto ya kuwa muuguzi, lakini baada ya kupata mimba nililazimika kuacha shule. Marafiki waliniacha na hata baadhi ya ndugu walinitenga ,” anasimulia kwa huzuni.Amina anasema ,hakuwahi kupata elimu ya kutosha kuhusu afya ya uzazi,
jambo ambalo linaonekana kuwa chanzo kikubwa cha tatizo kwa wasichana wengi hasa wa vijijini.
Kesi nyingine ni ya Zainabu (si jina lake halisi), msichana mwenye miaka 15 kutoka Nungwi, ambaye alipata
ujauzito baada ya kushawishiwa na mwanamme aliyemuahidi kumsaidia mahitaji yake
ya skuli.
“Nilikubali kwa sababu nyumbani hali ilikuwa ngumu ,Sikujua kama mwisho
wake ungekuwa hivi ,” anasema kwa masikitiko.
Kwa mujibu wa Mwalimu Mkuu wa Skuli ya Sekondari Matemwe Mkoa wa Kaskazini Unguja, Makame Sheha Mdacho,
tatizo hilo limekuwa likiongezeka mwaka hadi mwaka.
Anasema, baadhi ya wanafunzi wa
kike hushindwa kuendelea na masomo kutokana na mazingira magumu ya kifamilia
pamoja na ukosefu wa elimu sahihi ya afya ya uzazi.
Anasema kuwa, maeneo ya Matemwe vijana wadogo wa kiume wanamiliki dola, ( pesa za
kimarekani) kutokana na kuimarika kwa shughuli za kiutalii , hivyo imekuwa rahisi kuwarubuni Watoto wakike hasa wanafunzi ambao hawajajielewa na bado wako shuleni.
“ Skuli zimekuwa zikijaribu kutoa elimu ya maadili na afya ya uzazi kwa
wanafunzi , lakini bado juhudi zaidi zinahitajika kutoka kwa wazazi na jamii kwa ujumla ili kuhakikisha
Watoto wakike wanafikia ndoto zao za kielimu” amesema.
Nuru Abdalla, mzazi kutoka Shehia ya Matemwe Kusini anasema, mabadiliko ya teknolojia pamoja na matumizi
mabaya ya mitandao ya kijamii yamechangia kuongezeka kwa mimba za utotoni.
Anasema kuwa, baadhi ya watoto hutumia simu bila uangalizi,
hali inayowafanya kujiingiza katika mahusiano yasiyofaa mapema.
“Tunajaribu kuwaelekeza watoto wetu lakini mazingira ya sasa ni magumu Tunahitaji
ushirikiano mkubwa wa pamoja kati ya
wazazi na viongozi wetu wa Serikali ,” anasema.
Kwa upande wake Shinuna Said Mtaalamu wa Afya ya Uzazi kutoka Hospitali ya Mahonda Wilaya ya
Kaskazini ‘B’Unguja anasema mimba za utotoni zina madhara makubwa kiafya kwa
wasichana wadogo.
Anasema kuwa, wasichana wenye umri
mdogo wako katika hatari kubwa ya kupata matatizo wakati wa ujauzito na
kujifungua ukizingatia viungo vyao bado havijakomaa.
“Miili yao bado haijakomaa vizuri kubeba mimba, wengine hupata upungufu
wa damu, Presha ya mimba au hata matatizo wakati wa kujifungua,” anasema.
Aidha, ameeleza kuwa baadhi ya wasichana hupata msongo wa mawazo kutokana
na kukataliwa na familia au jamii baada ya kupata ujauzito .
Mtaalamu huyo , anaeleza umuhimu
wa kuwapa wasichana elimu sahihi kuhusu
afya ya uzazi, kuwajengea mazingira salama ya kujifunzia pamoja na kuwawezesha
kiuchumi wazazi kunaweza kusaidia kupunguza tatizo hilo.
Naye, Afisa wa Ustawi wa Jamii
kutoka Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja Tatma Adam anasema juhudi mbalimbali zimekuwa
zikichukuliwa ili kupunguza tatizo hilo, ikiwemo kutoa elimu kwa jamii,
kuwasaidia watoto waliopata changamoto pamoja na kushirikiana na taasisi
mbalimbali za kiraia.
Anasema ,tatizo la mimba za
utotoni linaendelea kuwa changamoto kubwa inayohitaji hatua za haraka. Bila
juhudi za pamoja, wasichana wengi wataendelea kunyimwa haki yao ya elimu na
fursa za kutimiza ndoto zao.
Sheikh Nahoda Haji kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja, anasema jamii ina
wajibu wa kuhakikisha watoto wanapata malezi bora pamoja na mafunzo ya maadili
tangu wakiwa wadogo.
“Mtoto wa kike anahitaji kulindwa na kupewa nafasi ya kutimiza ndoto zake,
kwani elimu ni msingi wa maisha yake ya
sasa na baadaye,” anasema.
Aidha, amehimiza kuacha kuwanyanyapaa wasichana waliopata ujauzito na badala yake kuwapa msaada wa kisaikolojia na kijamii ili waweze kuendelea na maisha yao na kuendelea na masomo yao.
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ ) ni Asasi inayotetea haki za wanawake na watoto , Afisa Programu wa kupambana na Ukatili na Unyanyasaji wa Mwanamke na Mtoto wa kike (VAWG) Asya Hakim amesisitiza umuhimu wa elimu ya afya ya uzazi kwa wanawake na wasichana pamoja na kuimarisha malezi ya watoto.Afisa huyo amesema kuwa, lengo la mradi huo ni kuwajengea uwezo waandishi
wa Habari kuripoti matukio mbali mbali
ya udhalilishaji hasa vijijini ambako bado wanajamii hawana uwelewa na mwamko
wa kuyaripoti.
Mradi huo, wa ‘ Tunaweza Pamoja ’ unaotekelezwa na UN Women kwa kushirikiana na TAMWA ZNZ ambao umefadhiliwa na Norway chini ya mpango wa Pamoja wa umoja wa Mataifa, unaolenga kujenga jamii yenye usawa na isiyovumilia ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.


Post a Comment