VIWANJA 300 KUREJESHWA SERIKALINI KATIKA SHEHIA TATU ZA MAKUNDUCHI KWA KUTOKUENDELEZWA
NA MARYAM NASSOR
ZAIDI ya viwanja 300
vilivyotolewa kwa wananchi wa maeneo ya Tasani, Mzuri na Kiongoni, Makunduchi
Mkoa wa Kusini Unguja, vinatarajiwa
kurejeshwa Serikalini kutokana na kutoviendeleza kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi
namba 12 ya mwaka 1992.
Akizungumza na waandishi
wa habari katika ziara maalum ya kutembelea viwanja hivyo, Katibu Mtendaji wa
Kamisheni ya Ardhi Zanzibar , Mussa Kombo Bakar, amesema baadhi ya
wananchi walipewa viwanja hivyo kwa ajili ya makaazi tangu mwaka 2000 hadi sasa havijaendelezwa.
Amesema, kwa mujibu wa
Sheria ya Ardhi namba 12 ya mwaka 1992, wananchi wanaopewa ardhi wanatakiwa kuviendeleza
ndani ya kipindi cha miaka miwili, na wakishindwa kufanya hivyo viwanja hivyo
vinaweza kurejeshwa Serikalini.
Aidha amesema kuwa ,
jukumu la Kamisheni hiyo ni kutembelea maeneo hayo na kuandaa ripoti kwa
Serikali ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa, akieleza kuwa Waziri mwenye
dhamana ya Ardhi amepewa mamlaka ya kufuta hati au mikataba ya ukodishaji wa
ardhi kwa kushauriana na Rais wa Zanzibar.
“Sisi kama wataalamu wa
ardhi jukumu letu ni kuipatia Serikali taarifa ili iweze kuchukua hatua za
kufuta hati hizo na kuwapatia wananchi wengine au taasisi zinazohitaji ardhi
hiyo,” amesema Katibu Mtendaji huyo.
Ameeleza kuwa ,zoezi hilo la kutembelea viwanja limeanza rasmi, kwa kuvitembelea viwanja vya shehia ya Tasani, Mzuri na Kiungoni ambavyo vilitolewa kwa zaidi ya miaka 25 vikiwa bado havijajengwa makaazi hadi sasa.
Aidha, amefafanua kuwa
tafsiri ya kuendeleza kiwanja ni kujenga makaazi ya kuishi, na si kujenga uzio
pekee kama baadhi ya wananchi wanavyofanya.
Naye Katibu wa Sheha wa
Mzuri, Makunduchi, Mohamed Issa amesema
amelipokea vyema agizo hilo na ameahidi kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu
wa kuendeleza viwanja walivyopewa.
Hata hivyo, amesema
changamoto kubwa inayojitokeza ni kwamba baadhi ya wamiliki wa viwanja hivyo
hawaishi katika maeneo husika, jambo linalofanya iwe vigumu kuwafikia kwa
urahisi.


Post a Comment