Mifumo ya kidijitali kuimarisha uwazi wa mikopo Zanzibar
Na Maryam Nassor
Teknolojia imeendelea kubadili jinsi taasisi za umma
zinavyotoa huduma kwa wananchi. Kwa kutumia mifumo ya kidijitali, huduma nyingi
zimekuwa rahisi kupatikana; zimeongeza uwazi na kupunguza urasimu.
Zanzibar nayo ina nafasi ya kutumia teknolojia kuimarisha usimamizi wa
mikopo ya maendeleo inayotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu
kupitia mfumo wa 4-4-2, ili kuhakikisha fursa hizo zinawafikia walengwa
kwa haki, uwazi na ufanisi.
Katika miaka ya hivi karibuni, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imeendelea kutekeleza mpango huo kwa lengo la kuongeza ushiriki wa makundi
maalumu katika shughuli za kiuchumi, kupunguza umaskini na kuchochea maendeleo
ya jamii.
Hata hivyo, pamoja na dhamira hiyo, changamoto za ukosefu wa uwazi,
ucheleweshaji wa majibu ya maombi, upatikanaji mdogo wa taarifa na kutokuwepo
kwa mfumo wa kidijitali wa kufuatilia maombi zimeendelea kujitokeza katika
maeneo mbalimbali.
Wadau wa maendeleo na wataalamu wa sera wanaamini kuwa matumizi ya
teknolojia yanaweza kubadili hali hiyo kwa kuongeza uwajibikaji wa taasisi
zinazotekeleza mpango huo na kujenga imani ya wananchi.
Mfumo wa kidijitali unaweza kuondoa malalamiko
Mchambuzi wa sera za Uchumi Zanzibar, Almass Mohamed, anasema
mfumo wa kidijitali unaweza kupunguza changamoto nyingi zinazohusiana na utoaji
wa mikopo.
"Mwombaji anatakiwa aweze kufuatilia maombi yake kwa kutumia simu au
tovuti. Aone lini maombi yamepokelewa, yako hatua gani, yameidhinishwa au
yamekataliwa pamoja na sababu zake. Huo ndio msingi wa uwazi."
Anaongeza kuwa, mfumo huo unapaswa kuwa na taarifa zinazoonyesha idadi ya
waombaji, walionufaika, fedha zilizotolewa kwa kila wilaya na shehia pamoja na kiwango cha marejesho ya mikopo.
Kwa mujibu wake, upatikanaji wa taarifa hizo utapunguza malalamiko ya
upendeleo na kuongeza imani ya wananchi kwa taasisi zinazotekeleza mpango huo.
Wadau wa maendeleo wataka uwazi zaidi
Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wanawake
wenye Ulemavu Zanzibar (JUWAUZA) inayojihusisha
na uwezeshaji wa wanawake, Salma Saadat, anasema wananchi wengi bado
hawajui kiasi cha fedha kinachotengwa kila mwaka wala namna kinavyogawiwa.
"Wananchi wakipata taarifa za wazi wataweza kuuliza maswali sahihi
na kufuatilia matumizi ya fedha za umma. Hiyo ndiyo tafsiri halisi ya
uwajibikaji."
Anashauri pia kuwa, kila halmashauri ichapishe taarifa za
kila robo mwaka zikionyesha kiasi cha fedha kilichotolewa, idadi ya wanufaika,
aina za biashara zilizofadhiliwa na kiwango cha marejesho ya mikopo.
UN Women: Uwezeshaji wa wanawake ni kichocheo cha ukuaji wa uchumi
Hoja za wataalamu hao zinaungwa mkono na UN Women. Katika makala
yake ya mwaka 2023 yenye kichwa Five Things to Accelerate Women's
Economic Empowerment, shirika hilo linaeleza kuwa wanawake duniani bado
wanakabiliwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa mitaji na huduma za kifedha,
hali inayozuia ukuaji wa biashara zao.
UN Women inakadiria kuwa, biashara ndogo na za kati zinazomilikiwa na
wanawake zinakabiliwa na pengo la upatikanaji wa mitaji linalofikia takribani dola
za Marekani trilioni 1.7 duniani.
Shirika hilo linaeleza kuwa kuziba pengo hilo kupitia sera bora, huduma
za kifedha jumuishi na matumizi ya teknolojia kunaweza kuongeza mapato ya
biashara zinazomilikiwa na wanawake kwa wastani wa asilimia 12 ifikapo mwaka
2030.
Aidha, UN Women inasisitiza kuwa uwekezaji katika teknolojia, elimu ya
fedha, taarifa sahihi na huduma za kifedha zinazowafikia wanawake ni miongoni
mwa njia muhimu za kuongeza ushiriki wao katika uchumi na kukuza maendeleo
endelevu.
Katika muktadha wa Zanzibar, wataalamu wanaamini kuwa mfumo
wa kidijitali wa usimamizi wa mikopo unaweza kuwa nyenzo muhimu ya kuwafikia
wanawake wengi zaidi, kupunguza gharama za kufuatilia huduma na kuongeza uwazi
katika utoaji wa mikopo ya 4-4-2.
Baraza la Wawakilishi lina wajibu wa kusimamia uwajibikaji
Mwakilishi wa Jimbo la Paje, Jaku Hashimu Ayoub, anasema Baraza la
Wawakilishi lina wajibu wa kuhakikisha fedha za umma zinazotengwa kwa ajili ya
uwezeshaji wa wananchi zinatumika kwa uwazi na ufanisi.
"Tunapaswa kuhoji bajeti zilizotengwa, fedha zilizotolewa na matokeo
yaliyopatikana. Wananchi wanahitaji kuona fedha zao zinaleta maendeleo
halisi."
Anasema matumizi ya mifumo ya kidijitali yatawawezesha wajumbe wa Baraza
kufanya ufuatiliaji kwa kutumia takwimu sahihi badala ya taarifa za jumla.
Wananchi wanataka mfumo unaoeleweka
Katika mahojiano na baadhi ya viongozi wa vikundi vya wanawake na vijana,
wengi walieleza kuwa changamoto kubwa ni kutokupata mrejesho kuhusu maombi yao
baada ya kuyawasilisha.
Mwenyekiti wa kikundi cha wanawake kutoka Kaskazini Unguja, Bi. Halima
Ali, anasema:
"Tunaomba mikopo lakini mara nyingi hatupati mrejesho. Mfumo wa simu
au mtandao ungeondoa usumbufu wa kufuatilia ofisi hadi ofisi."
Kwa upande wake, kijana mjasiriamali Ahmed Juma anasema mfumo wa
kidijitali ungepunguza gharama za usafiri na muda wa kufuatilia maombi.
"Tungepata pia elimu ya kutumia mifumo ya kujaza maombi ya mikopo
kwa njia ya mtandao. Hilo lingeongeza uelewa wetu na kurahisisha upatikanaji wa
mikopo."
Wataalamu wanapendekeza nini?
Mtaalamu wa sera na utawala bora Zanzibar, Hafidh Ibrahim, anasema
suluhisho la muda mrefu ni kuwekeza katika mifumo ya kisasa ya kidijitali.
Anapendekeza kuanzishwa kwa mfumo wa kufuatilia maombi ya mikopo kwa
kutumia simu na tovuti, kuchapishwa kwa takwimu za wanufaika kila robo mwaka na
kutoa sababu za kukubaliwa au kukataliwa kwa maombi ili kuongeza uwazi.
Aidha, anashauri kuanzishwa kwa mfumo wa kupokea malalamiko kwa njia ya
mtandao, kutoa mafunzo ya matumizi ya mifumo ya kidijitali kwa wanawake, vijana
na watu wenye ulemavu, pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya ZEEA,
halmashauri na Baraza la Wawakilishi.
"Teknolojia inaweza kuwa nyenzo muhimu ya kuhakikisha
wananchi wengi zaidi wanapata mikopo kwa haki, uwazi na kwa wakati."
Hitimisho
Mifumo ya kidijitali si suala la teknolojia pekee, bali ni nyenzo ya
kujenga uwajibikaji, uwazi na usawa katika utoaji wa huduma za umma.
Kwa Zanzibar, uwekezaji katika mfumo wa kisasa wa usimamizi wa mikopo
unaweza kuongeza imani ya wananchi, kupunguza malalamiko na kuhakikisha
wanawake, vijana na watu wenye ulemavu wanapata fursa zinazostahili.
Kadiri Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inavyoendelea kutekeleza sera za
uwezeshaji wa wananchi kiuchumi, matumizi ya teknolojia yanapaswa kwenda
sambamba na uchapishaji wa takwimu za utekelezaji, usimamizi madhubuti wa fedha
na ushiriki wa wananchi katika kufuatilia matumizi ya rasilimali za umma.
Kwa kufanya hivyo, mpango wa 4-4-2 unaweza kuwa mfano wa mafanikio katika
kujenga uchumi shirikishi unaowanufaisha wananchi wote na kuchochea maendeleo
endelevu ya Zanzibar.

Post a Comment