Mikopo ya Asilimia 10: Ahadi bado haijatimizwa kwa wote


Mikopo ya Asilimia 10: Ahadi bado haijatimizwa kwa wote,

-          Walitimiza masharti, lakini bado wanasubiri,

Na Maryam Nassor

Zaidi ya mwaka mmoja umepita tangu Khadija Abdalla na wenzake wa kikundi cha wanawake kutoka Shehia ya Mahonda, Wilaya ya Kaskazini 'B', Unguja, waanze kufuatilia mkopo wa asilimia 10 unaotolewa kupitia mfumo wa 4-4-2. Walisajili kikundi, wakafungua akaunti ya benki na kukamilisha masharti yote yaliyowekwa wakiamini wangepata mtaji wa kuendeleza shughuli zao za ujasiriamali.

Badala yake, wameendelea kusubiri bila kujua lini watafaidika na mpango huo.

Kila wanapofuatilia maombi yao, hupewa jibu lilelile:

"Jisajilini tena kwenye mfumo mpya wa kidijitali."

Kwa Khadija, majibu hayo yamekuwa yakijirudia kwa miezi mingi bila kupewa taarifa zinazoonyesha hatua iliyofikiwa au sababu ya kuchelewa kwa mkopo.

"Tuna hamu ya kupata mkopo huu ili kuendeleza shughuli zetu za ujasiriamali. Lakini mpaka leo bado hatujafanikiwa. Kila tunapoulizia tunaambiwa tujisajili tena kwenye mfumo wa kidijitali badala ya ule wa awali wa karatasi," anasema.

Simulizi yake si ya kipekee. Inaakisi hali inayowakabili wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar ambao, licha ya kutimiza masharti, bado hawajapatiwa mikopo au taarifa za kueleweka kuhusu maombi yao.

Maswali yanayohitaji majibu

Malalamiko ya wananchi yanaibua maswali muhimu. Mikopo hiyo inatolewa kwa utaratibu gani? Ni nani anayestahili kunufaika? Kwa nini baadhi ya vikundi hupata mikopo mapema huku vingine vikisubiri kwa muda mrefu bila maelezo ya wazi?

Maswali haya yanaonyesha umuhimu wa kuangalia kwa karibu utekelezaji wa mpango huu na kama kweli unatimiza lengo la kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Mikopo ya asilimia 10 ni mpango wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar unaolenga kuwawezesha wananchi kupitia sehemu ya mapato ya ndani ya halmashauri. Kupitia mfumo wa 4-4-2, asilimia nne ya fedha hutengwa kwa wanawake, asilimia nne kwa vijana na asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu.

Lengo lake ni kuongeza mitaji kwa makundi hayo, kukuza ajira, kupunguza umaskini na kuimarisha shughuli za uzalishaji mali.

Mpango huu umejengwa juu ya Sheria ya Serikali za Mitaa Na. 9 ya mwaka 2023 na Sheria ya Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Zanzibar (ZEEA) Na. 2 ya mwaka 2022, ambazo zinaelekeza halmashauri na ZEEA kusimamia utekelezaji wa programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Pamoja na msingi huo wa kisheria, simulizi za walengwa zinaonyesha bado kuna pengo kati ya matarajio ya wananchi na utekelezaji wa mpango.

Masharti yanayowakwamisha baadhi ya walengwa

Kwa watu wenye ulemavu, kuruhusiwa kuomba mikopo hata mmoja mmoja kulionekana kuongeza fursa za kunufaika. Hata hivyo, baadhi yao wanaona bado kuna masharti yanayowazuia.

Kassimu Mohamed, mkazi wa Mahonda mwenye ulemavu wa viungo, anasema anatamani kupata mtaji wa kuanzisha biashara lakini anakwama kutokana na sharti la kuwa tayari ana biashara kabla ya kupata mkopo.

"Nitaanzaje biashara wakati sina mtaji wala ajira? Kama kweli lengo ni kutuwezesha kiuchumi, basi tupewe mtaji pamoja na mafunzo ili nasi tuweze kujenga maisha yetu na familia zetu," anasema.

Kauli yake inaibua mjadala kuhusu iwapo masharti yaliyopo yanawafikia walengwa waliokusudiwa. Kwa baadhi yao, uwezeshaji wa kweli unapaswa kuanza kwa kuwasaidia wale wasio na mtaji wa kuanzisha shughuli za kiuchumi.

Vijana nao wanasubiri

Changamoto zinazowakabili wanawake na watu wenye ulemavu zinaonekana pia kwa vijana.

Omar Nassor anasema kikundi chao kilikamilisha taratibu zote za maombi, lakini hadi sasa hakijapatiwa mkopo wala maelezo yanayowapa uhakika wa lini watanufaika.

Anasema katika mazingira ambayo Serikali haiwezi kuwaajiri wananchi wote, mikopo ya asilimia 10 inapaswa kuwa fursa ya kuwasaidia vijana kujiajiri badala ya kuendelea kusubiri ajira rasmi.

"Tuko tayari kufanya biashara na kujikwamua kiuchumi, lakini kila tunapofuatilia tunaambiwa tuendelee kusubiri kwa sababu mifumo haijakaa sawa. Hali hii inatukatisha tamaa kwa sababu hatuna uhakika wa lini tutapata mkopo," anasema.

Kauli yake inaonyesha kuwa changamoto kubwa si ukosefu wa nia ya kufanya kazi, bali kutokuwa na uhakika wa lini ahadi ya uwezeshaji itageuka kuwa fursa halisi.

Majibu ya Mamlaka: Utekelezaji unaendelea

Malalamiko ya wananchi yanapowasilishwa kwa mamlaka, picha inayojitokeza ni kwamba mpango wa mikopo unaendelea kutekelezwa na tayari umewanufaisha baadhi ya walengwa.

Afisa Ustawi wa Jamii wa Wilaya ya Kaskazini 'B', Jina Mohamed Haji, anasema tangu mwaka 2022 hadi sasa vikundi 35 vimepatiwa mikopo. Kati ya hivyo, 27 ni vya wanawake, sita vya vijana na viwili vya watu wenye ulemavu.

Anasema pia Halmashauri imewasilisha zaidi ya shilingi milioni 952 kwa Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Zanzibar (ZEEA) kufikia Machi 31 mwaka huu kwa ajili ya kutekeleza mpango huo.

Hata hivyo, anakiri kuwa baadhi ya changamoto zimejitokeza, hususan katika mifumo ya benki inayotumika kusimamia marejesho ya mikopo. Kwa mujibu wake, hali hiyo imechangia baadhi ya malalamiko kutoka kwa wanufaika na waombaji.

Kutokana na changamoto hizo, anashauri kuendelea kuboresha mfumo wa usajili na utoaji wa huduma ili kurahisisha upatikanaji wa mikopo na kuongeza ufanisi wa programu.

ZEEA yatoa taswira ya mafanikio

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA na Uhusiano wa ZEEA, Gharib Said Gharib, anasema mamlaka hiyo ilianzishwa kuratibu programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi kupitia mafunzo na mikopo.

Anasema hadi sasa ZEEA imetoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 53.9 kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji.

Kwa mujibu wake, tangu mwaka 2024 kupitia mfumo wa 4-4-2, vikundi 20 vya vijana vimepatiwa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 220, vikundi 55 vya wanawake zaidi ya shilingi milioni 334.6 na vikundi 12 vya watu wenye ulemavu zaidi ya shilingi milioni 49.2.

Anasema takwimu hizo zinaonyesha kuwa mpango huo unaendelea kuwafikia walengwa na una uwezo mkubwa wa kubadili maisha ya wananchi endapo utasimamiwa kwa ufanisi na kuwafikia wahitaji kwa wakati.

Pamoja na mafanikio hayo, anakiri kuwa changamoto kubwa inayoikabili programu ni urejeshaji wa mikopo. Hata hivyo, anasema tathmini ya mwaka 2024 ilibaini kuwa zaidi ya asilimia 70 ya wanufaika wa programu ya Inuka wamefanikiwa kuzalisha ajira.

Tatizo haliko kwenye sheria

Kwa mujibu wa mtaalamu wa sheria kutoka Zanzibar, Almass Mohamed, changamoto kubwa haipo katika uwepo wa sheria, bali katika utekelezaji wake.

Anasema sheria zilizopo zimeweka msingi mzuri wa kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, lakini mafanikio ya programu yatategemea uwazi, usawa na uwajibikaji wa taasisi zinazozisimamia.

Kwa mtazamo wake, wananchi wanapaswa kupata taarifa sahihi kuhusu masharti, vigezo vya kupata mikopo na hatua za maombi yao ili kuondoa sintofahamu inayojitokeza.

"Serikali, halmashauri, ZEEA na wadau wote wana wajibu wa kuhakikisha mikopo ya asilimia 10 inawafikia walengwa na kutimiza lengo la kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kujenga uchumi imara na kuchangia maendeleo ya Zanzibar," anasema.

Kauli hiyo inaonyesha kuwa mafanikio ya mpango huu hayatategemea tu kiasi cha fedha kinachotengwa, bali pia namna taasisi zinavyowajibika katika kusimamia utoaji wake na kuwafikia walengwa kwa wakati.

Uwazi utaongeza imani ya wananchi

Simulizi za Khadija Abdalla, Kassimu Mohamed na Omar Nassor zinaonyesha matarajio makubwa ambayo wananchi wameyaweka kwenye mikopo ya asilimia 10. Kwao, mpango huu ni fursa ya kujenga maisha bora kupitia ujasiriamali na shughuli nyingine za uzalishaji mali.

Kwa upande mwingine, takwimu zilizotolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini 'B' pamoja na ZEEA zinaonyesha kuwa tayari makundi kadhaa yamenufaika na mpango huo. Hata hivyo, malalamiko ya baadhi ya waombaji yanaonyesha kuwa bado kuna haja ya kuimarisha utoaji wa taarifa, kurahisisha mifumo ya maombi na kuhakikisha waombaji wanapata mrejesho wa wakati kuhusu hatua za maombi yao.

Kuboresha maeneo hayo kutasaidia kujenga imani ya wananchi kwa programu na kupunguza sintofahamu kuhusu namna mikopo inavyotolewa.

 

Uwajibikaji ndiyo kipimo cha mafanikio

Mikopo ya asilimia 10 ni fursa muhimu ya kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa Zanzibar. Uwepo wa sheria, taasisi na fedha ni msingi muhimu, lakini mafanikio yake yatapimwa kwa uwezo wa mfumo kuwafikia walengwa kwa haki, uwazi na kwa wakati.

Wananchi wanahitaji kuona kuwa taratibu zilizowekwa zinafanya kazi kwa ufanisi, maombi yao yanapatiwa majibu kwa wakati na changamoto zinazojitokeza zinatatuliwa kwa uwazi. Hivyo ndivyo imani kwa programu itaongezeka na lengo la kupunguza umaskini kupitia uwezeshaji wa kiuchumi litafikiwa.

Kwa kuendelea kuboresha mawasiliano, kurahisisha mifumo ya maombi na kuimarisha uwajibikaji wa taasisi zinazosimamia mpango huu, mikopo ya asilimia 10 inaweza kuendelea kuwa chachu ya maendeleo jumuishi na kuwasaidia wananchi wengi zaidi kujenga uchumi imara na maisha yenye tija Zanzibar.

 

 

 

 

 



No comments

Powered by Blogger.