VIONGOZI WANAWAKE WATAKIWA KUWA NA MSHIKAMANO KUPANUA FURSA ZA UONGOZI

Na Maryam Nassor

VIONGOZI wanawake walio katika nafasi mbalimbali za uongozi wametakiwa kuweka mshikamano na kushirikiana bila kujali tofauti za vyama vyao vya siasa ili kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za maamuzi nchini.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ), Nairat Abdullah, wakati akifungua mafunzo ya siku mbili kwa madiwani wanawake na waratibu wa shehia yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chama hicho Tunguu Unguja.

 Mkurugenzi Nairat amesema, licha ya hatua zinazopigwa katika kuwawezesha wanawake, bado uwakilishi wao katika nafasi za uongozi ni mdogo, ukifikia asilimia 24 pekee, hali inayohitaji mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wanawake ili kuongeza idadi hiyo.

“Ni lazima tushirikiane kwa pamoja ili wanawake wengi zaidi wapate nafasi za uongozi bila kujali anatoka chama gani, Lengo letu ni kuona wanawake wakiongeza uwakilishi wetu  katika ngazi zote za maamuzi,” amesema.

Amesema kuwa,  wanawake waliopo katika nafasi za udiwani wanapaswa kujiandaa kugombea nafasi za juu zaidi, ikiwemo Ubunge na Uwakilishi katika uchaguzi wa mwaka 2026, akieleza kuwa hilo linawezekana endapo watajengewa uwezo na kujiamini.

Aidha, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo viongozi hao ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi, kuongeza kujiamini na kuwa viongozi wanaokubalika na jamii kwa kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Mkufunzi wa mafunzo hayo,  Dk Imane Duwe, amesema kiongozi bora ni mtumishi wa wananchi na si mtawala, hivyo viongozi wanawake wanapaswa kuweka mbele maslahi ya wananchi wanaowaongoza.

Aidha  amesisitiza, umuhimu wa viongozi wanawake kuzingatia maadili na kuvaa mavazi ya staha, akieleza kuwa wao ni kioo cha wanawake wengine wanaotarajia kuingia katika nafasi za uongozi.

“Sisi wanawake tunapaswa kuwa mfano mzuri wa kuigwa kwa mwenendo na mavazi yetu, kwa sababu tunawawakilisha wanawake wengi ambao bado hawajapata nafasi za uongozi,” amesema.

Naye, Diwani wa Wadi ya Mwanakwerekwe, Fatma Juma Jabu, amesema mafunzo hayo yatamuwezesha kuboresha huduma kwa wananchi wa wadi yake na kuahidi kuendelea kuwahudumia kwa uadilifu, uwazi na bila upendeleo.

Ameipongeza TAMWA ZNZ, kwa kuendelea kuwawezesha wanawake kupitia mafunzo mbalimbali yanayowaandaa kushika nafasi za uongozi, akisema wanawake wengi wamefanikiwa kutimiza ndoto zao kutokana na programu hizo.

Kwa upande wake, Diwani wa Wadi ya Kihinani, Bahati Ali Rashid, amesema mafunzo aliyoyapata kupitia TAMWA ZNZ mwaka uliopita yamechangia mafanikio yake ya kisiasa na kumwezesha kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Ameiomba ,TAMWA ZNZ kuendelea kuandaa mafunzo kama hayo ili kuwajengea uwezo viongozi wanawake zaidi na kuongeza ushiriki wao katika uongozi.

Mafunzo hayo ya siku mbili yameandaliwa na TAMWA ZNZ na yamewakutanisha madiwani wanawake kutoka wadi mbalimbali za Unguja pamoja na waratibu wa shehia, yakilenga kuimarisha uwezo wao wa uongozi, uwajibikaji na utoaji wa huduma kwa wananchi.

No comments

Powered by Blogger.