MAZINGIRA MAGUMU YANAVYOWANYIMA WATOTO WA KIKE HAKI YA ELIMU KASKAZINI 'B' UNGUJA

Na Maryam Nassor

Mapambazuko yanapoanza katika baadhi ya vijiji vya Wilaya ya Kaskazini 'B', Unguja, watoto wengi wa kike hawaanzi siku zao kwa kujiandaa kwenda skuli. Badala yake huanza kwa kuchota maji, kufagia, kuosha vyombo, kupika na kulea wadogo  kabla ya kushika daftari.

 Wengine hufika darasani wakiwa wamechoka, huku wengine wakikosa masomo kabisa kwa sababu ya majukumu ya nyumbani na shughuli za kilimo.

Haya ndiyo maisha ya watoto wengi wanaoishi katika mazingira magumu ya kiuchumi na kijamii, ambako umaskini na mtazamo wa jamii vinaendelea kuwanyima haki yao ya msingi ya kupata elimu.

Ingawa elimu ni haki ya kila mtoto, watoto wa kike bado wanaathirika zaidi kuliko wavulana. Mbali na kuhudhuria masomo, wanatarajiwa kutimiza majukumu mengi ya kifamilia.

 Wakati wa msimu wa kilimo, wengi hushiriki kulima, kupanda, kupalilia na kuvuna mazao, hali inayowafanya kukosa muda wa kujisomea na wakati mwingine kuacha shule kabisa.

Mkurugenzi wa Elimu Mbadala na Elimu ya Watu Wazima, Bi. Mashavu Ahmada Fakih, anasema Serikali imeendelea kuweka mikakati ya kuwasaidia watoto na vijana waliokatiza masomo kurejea katika mfumo wa elimu kupitia programu za elimu mbadala.

Akizungumza wakati wa kukabidhi baiskeli kwa wanafunzi wa kituo cha elimu mbadala Mkwajuni, alisema lengo ni kuwapa nafasi ya kujifunza kusoma, kuandika, kufanya hesabu na kupata stadi za maisha zitakazowasaidia kujitegemea.

"Tunaamini kuwa ujuzi hauzeeki ,Hata waliokatiza masomo bado wana nafasi ya kujifunza na kujenga maisha yao kupitia elimu na mafunzo ya ujasiriamali," alisema.

Afisa  Ustawi wa Jamii kutoka Wilaya ya Kaskazini 'B Unguja  Fatma  Ussi' alisema changamoto kubwa ni baadhi ya wazazi kutothamini elimu kwa kiwango kinachostahili. Kutokana na shughuli za utalii na utafutaji wa kipato, baadhi ya familia huwahusisha watoto katika kazi badala ya kuwahimiza kuendelea na masomo.

Alisema kuwa , kupitia kampeni za uhamasishaji katika shehia mbalimbali, vijana wengi waliokuwa wamekatiza masomo wamejitokeza na sasa wanaendelea na elimu pamoja na kujifunza stadi za maisha.

Mwalimu wa Skuli ya Msingi Mahonda, Abbass Hassan, alisema hali hiyo inaonekana kila siku darasani. Muda wa masomo unafika baadhi ya wanafunzi bado wako njiani hawajafika .

"Utamkuta mwanafunzi anafika saa mbili wakati vipindi tayari vimeanza. Ukimuuliza sababu anasema alikuwa anaosha vyombo nyumbani. Hii inaonesha kuwa mzigo wa kazi za nyumbani bado ni kikwazo kikubwa kwa elimu ya mtoto wa kike," alisema.

Aliongeza kuwa , wazazi wanapaswa kuwapa watoto muda wa kutosha wa kujifunza badala ya kuwabebesha majukumu yanayozidi uwezo wao.

Kwa upande wake, Sheha wa Donge Majenzi, Ali Keis Jailan, alisema bado kuna haja ya kuendelea kuielimisha jamii kuhusu umuhimu wa elimu, hasa kwa watoto wa kike.

"Jamii bado haijabadilika vya kutosha. Tunahitaji kuwahamasisha wazazi kutambua kuwa elimu ndiyo msingi wa maisha bora ya watoto wao," alisema.

Kwa Salha Muharam, safari ya elimu ilisimama baada ya kumaliza Kidato cha Nne kutokana na wazazi kushindwa kumudu gharama za masomo. Alibaki nyumbani akijishughulisha na kazi za nyumbani na kilimo kabla ya kujiunga na programu ya elimu mbadala.

"Nimepata nafasi nyingine ya kujifunza Leo ninaweza kusoma, kuandika na nimejifunza ujasiriamali  Nina matumaini ya kujiajiri na kujitegemea," alisema.

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010, inaelekeza Serikali kuhakikisha wananchi wote wanapata fursa sawa ya elimu bila ubaguzi wa kijinsia.

Hata hivyo, takwimu zinaonyesha bado kuna changamoto. Ripoti ya UNICEF kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar na NBS inaonyesha kuwa mwaka 2021 asilimia 7.6 ya watoto wenye umri wa miaka 5 hadi 17 walikuwa wakijihusisha na kazi. Aidha, asilimia 75.9 walikuwa wakifanya kazi za nyumbani kama kupika, kufua, kusafisha nyumba na kulea watoto, jambo linalopunguza muda wa kujifunza.

Mashirika ya kiraia pia yanaendelea kutetea haki ya mtoto wa kike kupata elimu. Mkurugenzi wa TAMWA Zanzibar, Nairat Abdullah, alisema watoto wa kike hukumbana na changamoto nyingi, zikiwemo umaskini, ukatili wa kijinsia na ukosefu wa ulinzi, hivyo wanapaswa kupewa fursa ya kuendelea na elimu bila vikwazo.

Alisisitiza kuwa, suluhisho si kuwapeleka watoto skuli pekee, bali ni kubadili mitazamo ya jamii kuhusu mgawanyo wa kazi za nyumbani na kuwajengea watoto mazingira salama ya kujifunza.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi wa Uwezeshaji wa Jamii kwa Ajili ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kutoka Idara ya Maendeleo ya Jamii Kanisa Katoliki Jimbo la Zanzibar, Sister Editha Asimwe, alisema wanaendelea kutoa mafunzo ya  uongozi na kwa viongozi wa shehia na utawala bora kwa wananchi ili wajenge utamaduni wa maamuzi shirikishi yanayolinda haki za watoto.

Naye Afisa Tathmini na Ufuatiliaji wa Idara ya Maendeleo ya Kanisa Katoliki Kanda ya Zanzibar, Msafiri Thomas Mombo, alisema mradi huo unalenga kujenga mazingira wezeshi ya upatikanaji wa haki, kuweka Mazingira wezeshi ya elimu Jumuishi na fursa za kiuchumi kwa watu wanaoishi katika mazingira magumu, wakiwemo, wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Alisema kupitia mradi huo wameandaa mikakati ya kuwasaidia watoto wenye Ulemavu kwa kuwapatia vifaa vya masomo na kuhamasisha jamii kuwekeza katika elimu badala ya kuwategemea watoto katika shughuli za uzalishaji.

 

No comments

Powered by Blogger.