MSAADA WA KISHERIA: TUMAINI JIPYA KWA WANANCHI KUPATA HAKI ZAO

Na Maryam Nassor

Kwa miaka mingi, wananchi wengi hasa wanaoishi maeneo ya vijijini wamekuwa wakishindwa kupata haki zao kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo umbali wa huduma za kisheria, gharama kubwa za kufuatilia kesi pamoja na uelewa mdogo wa sheria.

 Hali hiyo imekuwa ikichangia migogoro mingi ya ardhi, ndoa, mirathi na hata vitendo vya ukatili wa kijinsia kumalizwa kienyeji au kubaki bila kushughulikiwa.

Kutokana na hali hiyo, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuimarisha huduma za msaada wa kisheria ili kuhakikisha wananchi wote, bila kujali mahali wanapoishi au uwezo wao wa kifedha, wanapata haki kwa wakati, kwa usawa na kwa ufanisi.

Akizindua Awamu ya Pili ya Kampeni ya Kitaifa ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia katika Viwanja vya Maonesho Kizimbani Dole, Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan, alisema Serikali itaendelea kuboresha huduma hizo ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Alisema kampeni hiyo inalenga kuondoa vikwazo vya umbali, gharama na uelewa mdogo wa sheria kwa kupeleka huduma za msaada wa kisheria hadi katika ngazi za kata, vijiji, mitaa na shehia.

Aidha, alisema mafanikio ya awamu ya kwanza ya kampeni hiyo yalionesha umuhimu wa huduma hizo baada ya zaidi ya wananchi milioni nne kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kufikiwa na kunufaika nazo.

"Upatikanaji wa haki ni msingi wa utawala bora, amani na utulivu wa taifa, Hivyo ni wajibu wa Serikali na wadau wote kuhakikisha huduma hizi zinawafikia wananchi wengi zaidi, hususan wanaoishi maeneo ya pembezoni na makundi maalumu," alisema Dk. Mwinyi.

Kauli hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha sheria hazibaki vitabuni bali zinawafikia wananchi kwa vitendo kupitia elimu na usaidizi wa kisheria.

Kwa upande wake, Afisa Tathmini na Ufuatiliaji kutoka Mradi wa Uwezeshaji wa Upatikanaji wa Haki na Utawala Bora wa Kanisa Katoliki Kanda ya Zanzibar kwa ufadhili wa Misereor, Msafiri Thomas Mombo, alisema taasisi yao imekuwa ikishirikiana na wasaidizi wa sheria (Paralegals) katika kutoa elimu ya haki za kisheria kwa wananchi wa shehia tano ambazo ni shehia ya Mkataleni, Mahonda, Kitope, Donge Majenzi, Bubwini Misufini zilizopo wilaya ya Kaskazini 'B' Unguja.

Alisema, bado wananchi wengi hawana uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kudai haki zao na kupata misaada ya kisheria, jambo linalochangia baadhi ya matukio ya ukatili na udhalilishaji kutoripotiwa katika vyombo vya sheria na kusuluhishwa kwa njia zisizo za kisheria (Zisizo rasmi).

"Matukio mengi ya udhalilishaji hutokea katika maeneo ya vijijini ambako jamii bado haina uelewa wa kuyafikisha kwenye vyombo vya sheria ili hatua stahiki zichukuliwe. Elimu ndiyo silaha muhimu ya kubadilisha hali hiyo," alisema Msafiri.

Kwa mujibu wake, elimu ya msaada wa kisheria imeanza kuleta mabadiliko chanya kwa wananchi wengi ambao sasa wanaelewa mahali pa kupeleka malalamiko yao na namna ya kupata msaada bila gharama kubwa.

Naye Sheha wa Shehia ya Mahonda, Ali Issa Kinole, alisema huduma za msaada wa kisheria zimekuwa msaada mkubwa kwa wananchi wa eneo hilo, kwani zimechangia kupungua kwa migogoro ambayo hapo awali ilichukua muda mrefu kutatuliwa.

Alisema wananchi wengi sasa wanapata haki zao kupitia ushauri wa wataalamu wa sheria na kuwataka wale wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali kutafuta msaada mapema badala ya kusubiri migogoro kuwa mikubwa.

"Tumekuwa tukiwapa elimu wananchi wenye migogoro ya ardhi, ndoa, mirathi pamoja na kesi za udhalilishaji ili watafute ushauri wa kisheria mapema na haki ipatikane kwa wakati," alisema Kinole.

Kwa upande wake, Mratibu wa UN Women Kanda ya Zanzibar, Lucy Tesha, alisema kuna umuhimu mkubwa wa kuwawezesha wanawake na vijana kwa kuwapatia elimu ya haki zao na namna ya kuzidai.

Alisema takwimu zinaonesha kuwa wanawake na wasichana bado wanaendelea kuwa waathirika wakubwa wa vitendo vya ukatili wa kijinsia, hivyo elimu ya msaada wa kisheria ni nyenzo muhimu ya kuwapa ujasiri wa kuripoti matukio hayo na kupata haki.

"Tunahitaji jamii inayowajengea uwezo wanawake na vijana kujua haki zao na namna ya kuzitetea. Elimu hii ni muhimu katika kupunguza vitendo vya ukatili na kujenga jamii yenye usawa," alisema Tesha.

Kauli hiyo inaungwa mkono na mwananchi wa Mahonda, Asya Bakar, ambaye alisema elimu ya msaada wa kisheria inapaswa kuwa endelevu, hasa kwa vijana ambao mara nyingi ndio waathirika wakubwa wa vitendo vya ukatili.

Alisema mara nyingi ,jamii husikia taarifa za watoto kubakwa au kulawitiwa, lakini baadhi ya kesi hizo huishia kufichwa ndani ya familia kutokana na uoga, mila au kutokujua taratibu za kisheria.

"Kila siku tunasikia taarifa za watoto kubakwa au kulawitiwa, lakini kesi nyingi haziendi mahakamani kwa sababu baadhi ya familia hazina uelewa wa kutosha kuhusu haki zao na namna ya kuzidai," alisema Asya.

Wadau wa sekta ya sheria wanaamini kuwa mafanikio ya kampeni ya msaada wa kisheria yatategemea ushirikiano wa Serikali, viongozi wa jamii, taasisi za kiraia pamoja na wananchi wenyewe katika kuhakikisha elimu hiyo inaendelea kutolewa kwa makundi yote ya jamii.

Kwa kufanya hivyo, wananchi wengi zaidi wataweza kupata haki zao kwa wakati, kupunguza migogoro inayoweza kuzuilika na kujenga jamii inayozingatia misingi ya sheria, haki, usawa na utawala bora.

MWISHO

 

No comments

Powered by Blogger.