UTAWALA BORA NGUZO YA UPATIKANAJI WA HAKI KATIKA JAMII

Viongozi wa Mahkama wawasihi wananchi, kushirikiana katika kutoa Ushahidi ili haki ipatikane.

Na Maryam Nassor

Katika jamii yoyote inayoheshimu sheria, haki na usawa, utawala bora ni msingi muhimu unaowezesha wananchi kupata haki zao kwa wakati na kwa usawa.

 Utawala bora hujengwa kupitia uwajibikaji wa viongozi, ushirikishwaji wa wananchi, uwazi katika maamuzi pamoja na utendaji unaozingatia sheria.

Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, katika Ibara ya 13, inaeleza kuwa watu wote ni sawa mbele ya sheria na wana haki ya kulindwa kwa usawa na sheria. Aidha, Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 inasisitiza umuhimu wa kulindwa kwa haki za msingi za binadamu na kuimarishwa kwa utawala unaozingatia sheria.

Licha ya kuwepo kwa sheria na katiba hizo, bado wananchi wengi wa vijijini hukumbana na migogoro ya kifamilia, migogoro ya ardhi, ukatili wa kijinsia na changamoto nyingine zinazohitaji msaada wa viongozi wa shehia, wasaidizi wa sheria, Jeshi la Polisi na Mahakama ili kupata haki zao.

Akizungumza na mwandishi wa makala hii, Fatma Ali, mkaazi wa Mahonda Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja, anasema msaada wa viongozi wa shehia ulimwezesha kupata haki baada ya mgogoro wa muda mrefu wa mipaka ya kiwanja chake kati yake na jirani yake.

Anasema ,mgogoro huo ulidumu kwa zaidi ya mwaka mmoja na kusababisha ugomvi mkubwa kati ya familia hizo mbili.

“Tulikuwa hatusemezani kabisa ,Kila mmoja alidai eneo hilo ni lake  Tulipofika kwa Sheha alituita pande zote mbili, akatusikiliza na kutushauri kufuata taratibu za kisheria. Mwisho wa siku tulipata suluhu na sasa tunaendelea vizuri,” anasema Fatma.

Anaeleza kuwa, kama kusingekuwa na usimamizi mzuri wa viongozi wa shehia, mgogoro huo ungeweza kusababisha vurugu kubwa katika eneo lao.

Mbali na viongozi wa shehia, wasaidizi wa sheria wameendelea kuwa msaada mkubwa kwa wananchi wanaohitaji mwongozo wa kisheria.

Khamis Maalim kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja, anasema alipata msaada wa kisheria baada ya kunyimwa haki ya urithi wa mali za familia kwa madai kuwa yeye ni mlemavu.

“Nilikuwa sifahamu nifanye nini baada ya ndugu zangu kunitenga katika mgawanyo wa mali. Kupitia msaidizi wa sheria nilielekezwa taratibu za kufuata na nikapata nafasi ya kusikilizwa. Leo nimepata sehemu yangu ya urithi kwa mujibu wa sheria,” anasema Khamis.

Anasema, elimu ya sheria inayotolewa kwa wananchi imekuwa msaada mkubwa kwa watu wengi ambao awali hawakujua namna ya kudai haki zao.

Katika masuala ya ukatili wa kijinsia, Jeshi la Polisi limeendelea kuwa nguzo muhimu katika kulinda haki za waathirika. Kupitia Dawati la Jinsia na Watoto, waathirika wa vitendo vya ukatili hupata fursa ya kuripoti matukio yao na kufanyiwa uchunguzi kwa mujibu wa sheria.

Mwanamke mmoja aliyeomba kutotajwa jina lake kutokana na unyeti wa tukio lake, anasema alipata haki baada ya kuripoti tukio la ubakaji katika Kituo cha Polisi Mahonda.

“Nilikuwa naogopa kutoa taarifa kwa sababu nilihisi sitaaminiwa. Lakini nilipofika Polisi nilisikilizwa na kupewa msaada. Uchunguzi ulifanyika na kesi ikapelekwa Mahakamani. Hilo lilinipa matumaini kuwa sheria ipo kwa ajili ya kulinda haki zetu,” anasema.

Anaeleza kuwa, hatua ya kuripoti tukio hilo ilimsaidia yeye pamoja na waathirika wengine kupata ujasiri wa kusimama na kudai haki zao.

Kwa upande wake, Hakimu wa Mahakama ya Mkoa wa Kaskazini Unguja, Lusiano Makoe Nyengo, anasema Mahakama zimeendelea kuwa sehemu muhimu katika utoaji wa haki kwa wananchi, ambapo migogoro mbalimbali ya kijamii hupatiwa ufumbuzi kwa kuzingatia sheria na ushahidi uliopo.

“Ni vyema wananchi kushirikiana na Mahakama katika kutoa ushahidi pale wanapoleta kesi zao mahakamani, kwani bila ya ushirikiano ni vigumu kesi kuendelea kusikilizwa na hatimaye kupata hukumu stahiki,” anasema Lusiano.

Naye Msaidizi wa Sheria kutoka Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja, Shabani Sariboko Makarani, anaeleza kuwa ushirikiano kati ya viongozi wa shehia, wasaidizi wa sheria, Polisi, Mahakama na wananchi ni muhimu katika kujenga jamii inayoheshimu sheria na kuzingatia misingi ya utawala bora.

Hata hivyo, amesema  ukosefu wa utawala bora unaweza kusababisha madhara makubwa katika jamii. Miongoni mwa madhara hayo ni kuongezeka kwa migogoro, rushwa, ubaguzi, ukiukwaji wa haki za binadamu na kupungua kwa imani ya wananchi kwa taasisi za umma.

“Pale ambapo viongozi hawawajibiki ipasavyo au sheria hazitekelezwi kwa usawa, wananchi wengi hujikuta wakikosa haki zao. Hali hiyo inaweza kusababisha baadhi ya watu kujichukulia sheria mkononi, jambo ambalo huathiri amani na mshikamano wa jamii,” anasema.

Aidha, anasema ukosefu wa utawala bora unaweza kuwafanya waathirika wa vitendo vya ubakaji, ukatili wa kijinsia na migogoro mingine kushindwa kupata haki kwa wakati. Matokeo yake ni kuongezeka kwa maumivu kwa waathirika na kuendelea kwa vitendo vya uvunjifu wa sheria katika jamii.

Mchambuzi wa masuala ya utawala bora, Almass Mohamed, anasema kuimarisha elimu ya sheria kwa wananchi, kuongeza uwajibikaji wa viongozi na kuimarisha utendaji wa vyombo vya haki kutasaidia kupunguza changamoto zinazowakabili wananchi.

Anasema ,wananchi nao wanapaswa kushiriki kikamilifu katika kulinda utawala bora kwa kutoa taarifa za vitendo vya uhalifu, kuheshimu sheria na kushirikiana na viongozi pamoja na vyombo vya dola katika kutatua changamoto zinazojitokeza katika maeneo yao.

Naye, Afisa Tathmini na Ufuatiliaji kutoka  Mradi wa Uwezeshaji  wa haki za kibinadamu na Utawala bora kutoka  kanisa katoliki  Msafiri Thomas, amesema  wamechagua Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja kutekeleza  mradi huo kwa sababu wamegundua uwelewa wa wananchi bado ni mdogo  wananchi wengi hawajui haki zao .

Amesema, katika tathimini ya awali waliyoifanya wamegundua kuwa maswali ya haki za binadamu na utawala bora kwa  wananchi  wa wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja  uwelewa wao uko chini kabisa.

“Upatikanaji wa haki katika jamii unategemea uwepo wa utawala bora unaohusisha ushirikiano kati ya wananchi na taasisi zote zinazosimamia sheria,  ambapo misingi ya utawala bora inazingatiwa, wananchi hupata fursa ya kusikilizwa, kulindwa na kutendewa haki bila ubaguzi, jambo linalochangia kudumisha amani, maendeleo na mshikamano wa jamii” Amesisitiza .

MWISHO

 


No comments

Powered by Blogger.