Sheria Zipo, Utekelezaji Wakwamisha Ushiriki wa Wanawake Katika Uongozi Zanzibar
NA MARYAM NASSOR
MRATIBU wa Watetezi wa Mtandao wa Haki za Binadamu Zanzibar, Suleiman
Muyuni Baitan, amesema kuwa licha ya kuwepo kwa sheria, kanuni na dira
mbalimbali za maendeleo zinazolenga kuimarisha ushiriki wa wanawake katika
nafasi za uongozi, bado utekelezaji wake haujaridhisha.
Alisema hayo, katika Afisi za Mufti Mombasa wakati akiwasilisha ripoti ya
Mapungufu ya kisheria na kiutendaji yanayohusu haki za Wanawake na Ushiriki wao
katika uongozi na michakato ya kidemokrasia.
Baitan alisema kuwa, sheria nyingi zilizowekwa kwa ajili ya kumuwezesha
mwanamke kushiriki katika uongozi bado hazitekelezwi ipasavyo, Alitolea mfano
Sheria ya Halmashauri inayotaka wanawake wawe angalau asilimia 40 katika baadhi
ya nafasi za uongozi, lakini kiwango hicho bado hakijafikiwa.
Alisema kuwa , Utafiti waliofanya ulilenga kuchunguza sheria, taratibu na
kanuni mbalimbali ili kubaini namna zinavyomsaidia mwanamke kushiriki
kikamilifu katika kugombea na kushika nafasi za uongozi.
Aidha, alisema utafiti huo umeibua haja ya kufanya maboresho ya baadhi ya
sheria pamoja na kusimamia utekelezaji wa sheria zilizopo, kwani Zanzibar ina
sheria nyingi nzuri zinazolenga kuwawezesha wanawake kuwa viongozi.
"Tuna sheria na sera zenye maudhui mazuri, lakini changamoto kubwa
ipo katika utekelezaji wak,. Sheria nyingi zilizopo hazilazimishi mamlaka
husika kuhakikisha kiwango maalum cha wanawake kinafikiwa katika nafasi za
uongozi, wala hazielezi hatua zinazopaswa kuchukuliwa endapo kiwango hicho
hakitafikiwa," alisema Baitan.
Aliongeza kuwa, Katiba kupitia Ibara ya 12 na 13 inaelekeza kuhusu usawa
wa kijinsia, lakini bado kuna haja ya kujiuliza kama masharti hayo
yanatekelezwa kwa vitendo.
Alisema taasisi yao, itaendelea kutoa elimu kwa jamii na kuiomba Serikali
kusimamia kwa karibu utekelezaji wa sheria zilizopo pamoja na mikataba ya
kikanda na kimataifa, ikiwemo CEDAW na SADC, ili kuongeza ushiriki wa wanawake
katika nafasi za uongozi.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi wa SWIL kutoka ZAFELA, Mwanaisha
Mustafa Makame, alisema lengo la kikao hicho lilikuwa kuwasilisha ripoti hiyo
kwa wadau mbalimbali ili kujadili yaliyobainishwa na kuanza kuyafanyia kazi.
Alisema ripoti hiyo, imeonesha mapungufu mbalimbali katika baadhi ya
sheria zilizopo, ikiwemo sheria zinazohusiana na gharama za uchaguzi ambazo
zimekuwa kikwazo kwa wanawake wengi wanaotaka kugombea nafasi za uongozi.
Naye Kiongozi wa Wanawake wa Chama cha ACT-Wazalendo, Halima Ibrahim,
alisema wanawake bado wanakumbana na vikwazo vingi katika harakati za kutafuta
nafasi za uongozi na kuwataka wadau kushirikiana katika kuweka mazingira salama
na yenye usawa kwa wote.
Alisema kuwa, wanawake wengi wana
hamasa ya kugombea nafasi za uongozi, lakini hukumbwa na changamoto mbalimbali,
ikiwemo ukosefu wa rasilimali za kifedha za kugharamia kampeni na shughuli za
uchaguzi.
Kikao hicho cha uwasilishaji wa Ripoti ya Mapungufu ya Kisheria na Kiutendaji kimeandaliwa na Chama cha Wanasheria Wanawake Zanzibar ( ZAFELA) na kiliwakutanisha wadau mbalimbali, wakiwemo viongozi wa Vyama vya Siasa, Maafisa kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
pamoja na wawakilishi wa asasi za kiraia, kwa lengo la kujadili changamoto
zilizobainishwa na kutafuta suluhisho litakalowezesha wanawake kushiriki
kikamilifu katika uongozi na michakato ya kidemokrasia.
MWISHO
Post a Comment