SERIKALI IWEKE WAZI RATIBA YA KUWASILISHA MSWADA WA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI ZANZIBAR - ZAMECO

NA MARYAM NASSOR

KAMATI ya Wataalamu wa Masuala ya Habari Zanzibar (ZAMECO) inaishauri Serikali kuharakisha taratibu za kuuwasilisha Barazani Mswada wa Huduma za Habari Zanzibar ili ujadiliwe na kuwa sheria, mswada ambao umekuwa ukipigwa dana ,dana kwa zaidi ya miaka kumi sasa.

 Sheria za Habari zimepitwa na wakati, na zinapatikana katika vipande vipande vikiwemo katika Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu Na. 5 ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na Sheria Na. 7 ya mwaka 1997, Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar Na. 7 ya mwaka 1997 iliyofanyiwa marekebisho na Sheria Na. 1 ya mwaka 2010, Sheria Na. 6 ya Baraza la Wawakilishi ya mwaka 2022 na Sheria ya Kufuta Sheria ya Uchaguzi Na. 11 ya mwaka 1984 na Kutunga Sheria ya Uchaguzi ya 2017 na Mambo Yanayohusiasa na Hayo

Sheria hizi zimezipa nguvu kubwa taasisi za Serikali ikiwemo kusajili na kufungia vyombo vya habari kinyume na maelekezo ya demokrasia yanayosisitiza ushirikishaji na utawala bora wa sheria.

Taarifa kwamba Mswada huo, upo tayari na unatarajiwa kufikishwa Barazani zilianza kusikika tokea Balozi Mahmoud Thabit Kombo alipokuwa Waziri wa Habari mwaka 2015. Mei 2023 wakati wa maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Habari, aliyekuwa Waziri wa Habari; Bi Tabia Maulid Mwita alitangaza kuwa Mswada huo ulishakamilika kwa asilimia 80 mbele ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe Dkt. Hussein Mwinyi.

Naye Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Dkt.Riziki Pembe wakati wa kikao chake cha kwanza na wadau wa sekta ya Habari cha tarehe 28 Januari 2026 aliwaambia waandishi wa Habari kuwa anatarajia kuuwasilisha Barazani Mswada wa sheria hiyo ifikapo Septemba mwaka huu.

Hadi sasa, Bajeti ya Wizara ya Habari ya 2026/27 imeshapitishwa na kugusia tu kutayarisha sera, sheria na kanuni mbali mbali zinazojumuisha Wizara hiyo, lakini haikuzungumzia kwa upekee juu ya mswaada wa Sheria ya Habari Zanzibar.

ZAMECO imefuatilia kwa karibu mjadala uliofanyika katika Kikao cha 11 cha Mkutano wa Tatu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, kilichoanza Mei 6, 2026, ambao utamalizika rasmi baada ya kukamilisha shughuli zake za bajeti.

Wakati wa mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Habari, Wawakilishi kadhaa waliitaka Serikali kueleza kwa uwazi lini sheria hiyo itawasilishwa rasmi Barazani.

Wajumbe waliochangia walionesha kutoridhishwa na ucheleweshaji wa muda mrefu wa sheria hiyo, huku mmoja wao akisema: “Sheria ya habari imefikia wapi? Waandishi wa habari wamesema mpaka wamechoka, sheria imekuwa ikitolewa ahadi tu italetwa Barazani lakini ni hadithi tu haifiki, miaka imekuwa mingi.” Mhe. Jaku Hashim Ayoub, Mwakilishi jimbo la Paje.

"Sheria ya habari imekuwa ikiahidiwa kwa muda mrefu kuwasilishwa Barazani, lakini hadi sasa bado haijafikishwa. Tunahitaji kuambiwa wazi ni lini hasa Serikali italeta sheria hiyo katika Baraza la Wawakilishi ili tuweze kuijadili na kuifanyia maamuzi. Wananchi na wadau wa sekta ya habari wanastahili kupata majibu ya uhakika badala ya kuendelea kusikia ahadi zinazojirudia." Prof. Omar Fakih, Mwakilishi wa Jimbo la Pandani

ZAMECO inawapongeza, wawakilishi wote ambao kwa dhati kabisa wamepokea kilio cha muda mrefu cha wadau wa habari na kukifikisha kilio hicho ndani ya Baraza la Wawakilishi kwa weledi mkubwa.

Ni wazi kuwa, sheria ya huduma za habari ikipitishwa haitawalinda waandishi wa habari pekee bali jamii kwa ujumla na kuharakisha maendeleo ya nchi kiuchumi, kisiasa na kijamii kwa vile itasimamia uongozi bora ikiwemo mapambano dhidi ya rushwa, haki, usawa, uwazi na uwajibikaji.

 “Sheria ya sasa imepitwa na wakati na inahitaji maboresho ya haraka ili kuendana na maendeleo ya sekta ya habari na teknolojia”, Mhe. Seif Hamad (Jimbo la Ole) na Mhe. Said Ali Mbarouk (Jimbo la Gando), ambaye pia aliwahi kuwa Waziri wa Habari mwaka 2010, walisisitiza.

Michango hiyo ya Wawakilishi inaonesha, uelewa mkubwa kuhusu mchango wa sekta ya habari na zinaakisi sauti na matarajio ya wadau wengi wa habari sababu sheria hiyo italinda haki ya kutoa taarifa, kupata taarifa na uhuru wa kujieleza ambazo ni haki za msingi za binadamu kama zilivyoainishwa katika mikataba mingi ya kimataifa, kikanda na kitaifa.  Hii ni pamoja na;

Ibara ya 19 ya Azimio la Kimataifa la Haki za Binaadamu (UDHR), Ibara ya 9 ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binaadamu na Watu (ACHPR), Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (ICCPR), pamoja na Katiba ya Zanzibar na Tanzania.

Kamati pia imebaini kuwa, pamoja na umuhimu wa maboresho ya sheria, bado kuna changamoto zinazowakabili waandishi wa habari katika utekelezaji wa majukumu yao. Miongoni mwa changamoto hizo ni mazingira yasiyoridhisha ya kufanyia kazi waandishi wanaoripoti shughuli za Baraza la Wawakilishi, jambo ambalo lilielezwa na baadhi ya wajumbe kuwa linahitaji kupatiwa ufumbuzi wa haraka.

ZAMECO inaamini kuwa, kuboresha mazingira ya kazi kwa waandishi wa habari ni sehemu muhimu ya kuimarisha taaluma ya habari, kuongeza ubora wa taarifa zinazowafikia wananchi na kuwezesha vyombo vya habari kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi zaidi.

Kamati inaona kuwa, Zanzibar yenye maendeleo, uwazi na usawa inahitaji mazingira salama ya kisheria na kiutendaji yatakayowezesha waandishi wa habari na vyombo vya habari kutekeleza wajibu wao kwa uhuru, weledi na bila vitisho. Aidha, uandishi wa habari za uchunguzi unapaswa kupewa nafasi na ulinzi wa kutosha kutokana na mchango wake katika kufichua ukweli, kulinda rasilimali za umma na kuimarisha uwajibikaji.

ZAMECO inaiomba tena, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuharakisha mchakato wa kukamilisha na kuwasilisha Mswada huo Septemba mwaka huu kama ilivyoahidiwa ambapo inaamini kuwa Sheria ya Huduma za Habari itajenga mfumo wa kisheria unaokwenda sambamba na mabadiliko ya kidijitali, unaolinda uhuru wa habari, unaokuza uwajibikaji na unaochangia maendeleo ya sekta ya habari nchini. Wakati huo huo, Kamati inawahimiza waandishi wa habari kuendelea kuzingatia maadili ya taaluma yao, ikiwemo uadilifu, usahihi, uwajibikaji na uzingatiaji wa maslahi ya umma.

ZAMECO inajumuisha mashirika yanayojihusisha na masuala ya habari, waandishi wa habari, wahariri, pamoja na Mtandao ya utetezi wa haki za binaadamu nchini.

IMETOLEWA NA:

Chama Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC),

Cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA-ZNZ),

Waandishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA),

Baraza la Habari Tanzania, Zanzibar (MCT, ZNZ),

Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania, Zanzibar (THRDC, ZNZ).



 

 

 

 

 


No comments

Powered by Blogger.