RUSHWA MUHALI NI SUALA LILILOPITWA NA WAKATI - TAMWA ZNZ


NA MARYAM NASSOR

MKURUGENZI wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ)Nairat Abdulla Ali  amesema rushwa  muhali ni suala lililopitwa na wakati na kuitaka jamii kushirikiana pamoja  ili kuwanusuru manusura wa vitendo hivyo.

Akizungumza katika ukumbi wa chama hicho uliopo Tunguu, Unguja, wakati wa kikao na wadau wa mtandao wa kupinga udhalilishaji Zanzibar, amesema kuwa vitendo vya rushwa ya  muhali vinaathiri kwa kiasi kikubwa ustawi wa wanawake na wasichana, hususan katika maeneo ya vijijinii.

Ameeleza kuwa, licha ya jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali, bado baadhi ya wahusika wanatumia nafasi zao vibaya kwa kuomba au kushinikiza rushwa  muhali, jambo linalodumaza haki na usawa katika jamii.

Akibainisha kuwa“ ukimya unaochangiwa na hofu na unyanyapaa umekuwa kikwazo kikubwa katika mapambano dhidi ya vitendo hivyo” amesema .

Aidha, amesisitiza umuhimu wa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa kuhusu haki za msingi na madhara yanayowapata wanawake na wasichana .

Kwa upande wake Manager  wa kitengo cha mawasiliano kutoka TAMWA ZNZ  Bi Sophie Ngalapy. amesisitiza  umuhimu wa kuheshimiana mkubwa kumuheshimu mdogo na mdogo kumuheshimu  mkubwa ili kujiepusha na vitendo vya udhalilishaji .

Amesema kuwa, elimu  ni muhimu sana katika kukabiliana na vitendo vya udhalilishaji  katika jamii ili kumaliza matendo haya nchini.

Kwa upande wake, mmoja wa  wasaidizi wa sheria  wilaya ya kaskazini ‘A’ Unguja Asya  Fadhil Makame amesema kuwa kuna haja ya kuimarisha mifumo ya kuripoti matukio ya udhalilishaji ili manusura waweze kupata msaada wa haraka na haki stahiki bila kuogopa.

Ameongeza kuwa,  ushirikiano kati ya taasisi za serikali, asasi za kiraia na jamii kwa ujumla ni muhimu katika kuhakikisha vitendo vya rushwa ya  muhali vinatokomezwa kabisa.

 Naye, mwakilishi wa Un Women Tanzania kwa upande wa Zanzibar Jesca Msafiri  amesema,  vitendo vya udhalilishaji  vinahitaji ushirikiano wa Pamoja kati ya Serikali na wadau mbali mbali.

Amesema,  takwimu za vitendo vya udhalilishaji  Tanzania vinaonesha kwa kila wanawake 40   wanne wamefanyiwa vitendo hivyo,  na kila wanaume 10 mmoja amefanyiwa vitendo vya udhalilishaji.

“ Takwimu hizi ni kwa wale wanaoripoti  matendo  haya, lakini baadhi ya wanajamii bado hawaripoti vitendo vya udhalilishaji   kutokana na kukosa elimu na  muhali” amesema.

 Nao , washiriki wa kikao hicho  wamependekeza kuanzishwa kwa kampeni endelevu zitakazolenga kubadili mitazamo hasi ya jamii pamoja na kuwajengea uwezo wanawake na wasichana kujitambua na kujilinda dhidi ya vitendo vya udhalilishaji.



No comments

Powered by Blogger.